Akavitia vitu vyote chini ya miguu yake, akamweka awe kichwa juu ya vitu vyote kwa ajili ya kanisa; ambalo ndilo mwili wake, ukamilifu wake anayekamilika kwa vyote katika vyote (Waefeso 1:22-23).
Andiko letu la ufunguzi lina nguvu sana, na lenye kufunua. Kanisa ni ukamilifu wa Kristo! Hilo lina maana kuwa sisi tu utimilifu wa Kristo; Yeye ni kichwa, na sisi tu mwili, na unapotuweka pamoja, sisi ni Kristo katika utimilifu. Sisi ni utimilifu Wake ambaye Amekamilika kwa vyote na katika vyote. Kweli iliyobarikiwa! Ninatamani watoto wote wa Mungu waweze kuidaka hii!
Yohana 1:16 inasema, “Kwa kuwa katika utimilifu wake sisi sote tulipokea, na neema juu ya neema.” Tumepokea utimilifu Wake wote! Ndio maana siyo ajabu Yesu alisema katika Yohana 5:26, “Maana kama vile Baba alivyo na uzima nafsini mwake, vivyo hivyo alimpa na Mwana kuwa na uzima nafsini mwake”; Alikuwa akizungumza juu ya uzima wa kurithi. Amejawa na uzima; Ana uzima wote; Uungu wote. Mungu Baba hana uzima zaidi kuliko ule alionao Yesu. Kisha, tunasoma katika Yohana 1:16 kwamba tumepokea utimilifu Wake. Amejawa na uzima, amejawa na Mungu, na utimifu huo umepasishwa kwetu, sio kwa vipande vipande, bali kwa utoshelevu (ujazo) wote! Endapo tungekuwa na uzima kidogo kuliko Alionao, tusingekuwa utimilifu Wake, kwa sababu Maandiko yanasema, “…kwa ajili ya kanisa; ambalo ndilo mwili wake, ukamilifu wake anayekamilika kwa vyote katika vyote.” Kila mmoja wetu amejazwa ndani Yake, na pamoja Naye. U ndani Yake, na Yeye yu ndani yako. Huu ulikuwa ndiyo mpango wa Mungu, wazo, na ndoto Yake tokea kabla ya kuumbwa kwa misingi ya ulimwengu, kwetu sisi kuwa utimilifu wa Kristo, na Alilitimiza hilo katika Kristo Yesu, na kwa kumtuma Roho Mtakatifu kuja kuishi ndani yetu.
Kanisa ni mwili wa kupita kawaida [mwili wa kimiujiza]; na wewe ni sehemu ya mwili huo. Umejawa na Mungu, na sio magonjwa na maradhi. Inawezekana kuwa uliwahi kuambiwa kwamba ulizaliwa kutoka katika familia masikini, hivyo, inawezekana usiwe na mafanikio makubwa katika maisha; lakini hilo haliwezekani, kwa sababu unatokana na familia nyingine; familia ya Kristo—yaani Kanisa! Na katika Kristo, u katika utajiri, fahari, usitawi, na utukufu. Haleluya!
