Ndugu zangu, nawasihi, waangalieni wale wafanyao fitina na mambo ya kukwaza kinyume cha mafundisho mliyojifunza; mkajiepushe nao (Warumi 16:17).
Andiko letu hapo juu linatuasa kuwatambua na kujiepusha na wale wanaosababisha matengano [fitina] na wenye kukwaza kinyume cha mafundisho ya Kristo. Umefundishwa pendo la Kristo; umefunzwa na Neno la Mungu katika njia yaani uelekeo fulani; endelea katika Neno; weka alama na jiepushe na wale wanaoishi kinyume cha kweli ya Injili; kweli ambayo umefundishwa. Haya ni maagizo ya Mungu. Ni onyo lile lile Alilolitoa kupitia Mtume Paulo kwa Kanisa la Wafilipi; alisema, “Jihadharini na mbwa, jihadharini na watendao mabaya, jihadharini na wajikatao" (Wafilipi 3:2).
Sasa, onyo hili kwanza kabisa ni kukaa mbali na wale ambao wapo kanisani lakini hawaifuati kweli, ambao wanasababisha magomvi na fitina. Pindi unapoona kiashiria katika nyumba ambacho kinasema, “Tahadhari kuna mbwa wakali,” kiashiria hicho hakikuhabarishi juu ya mbwa nje ya nyumba hiyo, bali mbwa walio ndani katika nyumba hiyo. Hivyo, pindi Mtume Paulo aliposema, “Jihadharini na mbwa, jihadharini na watendao mabaya, jihadharini na wajikatao” alikuwa akimaanisha watu wenye kusababisha fitina [hila] walio ndani ya Kanisa.
Hawa wanaweza kuwa ni watu katika Kanisa unakosali [Kanisa la mtaani kwako], seli iyo hiyo, mtaa uo huo, kaya iyo hiyo, ofisi, n.k., na ni Wakristo. Asingekuonya kuwa na tahadhari na watu hao endapo Asingeona kuwa mahusiano yao pamoja nawe yasingekuwa na madhara katika mwenendo wako wa Kikristo. Wengi wamejikuta katika tafrani kubwa kwa kujihusisha na watu wasio sahihi. Onyo la Bwana liko wazi: kwamba “wamaki” na “jiepushe” na watu wenye kusababisha fitina, na sio kujaribu kuwabadilisha. Usiwe na ushirikiano na watu ambao kwa makusudi hawatembei katika upendo, watu wanaosabisha mafarakano ndani ya Kanisa; watu wenye hulka ya kuwapotosha wengine.
Watu hujikuta katika mikanganyiko pindi wanapojihusisha na mtu mwenye mkanganyiko. 1 Wakorintho 15:33 unasema, “Msidanganyike; Mazungumzo mabaya huharibu tabia njema.” Endapo ulikuwa na, au una marafiki ambao katika kujihusisha nao hujaona maendeleo yo yote ya kiroho, au kupitia urafiki wao umedhoofisha ufanisi wako katika Injili, ni wakati wa kuachana na urafiki wa namna hiyo. Usijiulize mara mbili [usijadili]; bali sitisha urafiki huo, ili ushiriki wako katika imani—maisha yako ya Kikristo—yawe na ufanisi kama vile yanavyopaswa kuwa. Utukufu kwa Mungu!
